Tanzania emblem
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Ofisi ya Katibu Mkuu Kiongozi

Habari

Leo tarehe 14 Machi, 2017, Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi Mha. John W.H. Kijazi, amekutana kwa mazungumzo na wadau wa sukari nchini.


KATIBU MKUU KIONGOZI AKUTANA NA WADAU WA SUKARI NCHINI

Leo tarehe 14 Machi, 2017, Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi Mha. John W.H. Kijazi, amekutana kwa mazungumzo na wadau wa sukari nchini. Wadau hao ni kutoka katika Bodi ya Sukari Tanzania; Chama cha Wazalisha Sukari Tanzania; na Chama cha Wakulima wa Miwa Tanzania.

Wengine walioshiriki ni kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera na Uratibu); Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi (Kilimo); Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji; na Kituo cha Uwekezaji nchini.

Pamoja na mambo mengine, Kikao kimejadili maendeleo ya sekta ya sukari nchini na kutathmini hali ya upatikanaji wa sukari kuanzia mwezi Julai 2016 hadi mwishoni mwa mwezi Februari 2017. Aidha, wadau wamejadili suala la utekelezaji wa maelekezo ya Serikali kwa wazalishaji wa sukari kuongeza uzalishaji ili kukidhi mahitaji ya soko la ndani.

Katibu Mkuu Kiongozi amewataka wadau wote, hususan Wazalishaji wa Sukari na Wakulima wa Miwa kushirikiana katika kutimiza azma ya Serikali ya kuhakikisha upatikanaji wa sukari ya kutosha kwa matumizi ya ndani.

Aidha, amemtaka Katibu Mkuu anayeshughulikia Kilimo kukutana na wadau hao kuzungumzia changamoto mbalimbali zinazowakabili na kupata maoni yao ya namna ya kuzipatia ufumbuzi.

Wawakilishi wa Wazalishaji wa Sukari na Wakulima wa Miwa nchini wamemshukuru Katibu Mkuu Kiongozi kwa kukutana nao. Aidha, wamemuahidi kutoa ushirikiano kwa Serikali katika ujenzi wa sekta imara ya sukari nchini.