Tanzania emblem
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Ofisi ya Katibu Mkuu Kiongozi

Habari

Katibu Mkuu Kiongozi na Mwenyekiti wa Kamati ya Utendaji ya Baraza la Taifa la Biashara, Balozi Mha. John W. H. Kijazi aongoza Mkutano wa 32 wa Kamati ya Utendaji ya Baraza hilo jijini Dar es Salaam.


Leo tarehe 23 Septemba, 2016, Katibu Mkuu Kiongozi na Mwenyekiti wa Kamati ya Utendaji ya Baraza la Taifa la Biashara (TNBC) Balozi Mha. John W. H. Kijazi ameongoza Mkutano wa Kamati Tendaji wa Baraza hilo uliofanyika kwenye ukumbi wa mikutano wa Ofisi za Baraza zilizopo katika Jengo la TANHOUSE, barabara ya Ali Hassan Mwinyi Dar es Salaam.

Mkutano huo ni wa kwanza kufanyika tangu Wajumbe wa Baraza hilo wapatao 40 (20 kutoka sekta binafsi na 20 kutoka sekta ya umma) wateuliwe na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dk. John Pombe Joseph Magufuli mapema mwaka huu.

Katika majadiliano hayo, wawakilishi wa sekta binafsi wakiongozwa na Mwenyekiti Mwenza, Dk. Reginald Mengi, Mwenyekiti Mtendaji wa IPP walisisitiza umuhimu wa mahusiano ya karibu baina ya Serikali na sekta hiyo na hivyo kupongeza uamuzi wa kufanyika kwa Mkutano huo. Aidha, walipongeza hatua mbalimbali za Serikali zenye lengo la kuweka mazingira mazuri zaidi kwa biashara na uwekezaji nchini, hususan uwekezaji wa ndani. Vilevile waliahidi kuendelea kuunga mkono azma ya Serikali ya kujenga nchi ya uchumi wa viwanda, suala ambalo wamependekeza liwe ni mada kuu katika Mkutano ujao wa Baraza hilo.

Akizungumza katika Mkutano huo, Mwenyekiti wa Kamati ya Utendaji, Balozi Mha. John W. H. Kijazi aliwashukuru Wajumbe kutoka sekta binafsi kwa kuteuliwa kuwawakilisha wafanyabiashara wenzao katika Baraza hilo. Aidha, aliwahakikishia kuwa Serikali inaheshimu na itaendelea kudumisha mahusiano chanya baina yake na sekta binafsi, kwani inatambua umuhimu wa sekta hiyo katika ujenzi wa taifa. Vilevile, alisisitiza umuhimu wa kutumia jukwaa hilo kuweka mikakati ya pamoja na kuendeleza sekta ya biashara na kukabiliana na changamoto zinazoikabili.

Baraza la Taifa la Biashara lilianzishwa kwa Waraka wa Rais Na. 1 wa mwaka 2001 likiwa na jukwaa mahsusi la majadiliano baina ya sekta binafsi na sekta ya umma. Vilevile, Baraza liliundwa kwa lengo la kuhamasisha uboreshaji wa mazingira ya biashara na uwekezaji, wa ndani na nje; pamoja na suala zima la maendeleo ya sekta binafsi ambayo ni mhimili muhimu katika ukuaji wa uchumi na maendeleo ya nchi kwa ujumla.

Kamati ya Utendaji, ni sehemu muhimu ya Baraza hilo yenye jukumu la kusimamia utendaji wa kila siku wa Baraza. Kamata hukutana mara nne kwa mwaka kwa lengo la kupokea taarifa ya utekelezaji wa maazimio yaliyopitishwa kwenye mikutano iliyotangulia, ikiwemo Mikutano ya Baraza la Taifa la Biashara.