Habari
Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi John W.H. Kijazi, leo tarehe 9 Machi, 2016 amekutana kwa mazungumzo na Mwenyekiti wa Bodi ya Taasisi ya Uongozi, Balozi Kari Alanko.
Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi John W.H. Kijazi, leo tarehe 9 Machi, 2016 amekutana kwa mazungumzo na Mwenyekiti wa Bodi ya Taasisi ya Uongozi, alipomtembelea Ofisini kwake akifuatana na Mtendaji Mkuu wa Taasisi hiyo, Prof. Joseph Semboja na Balozi wa Finland nchini, Mhe. Pekka Hukka.
Kwa
ujumla, mazungumzo hayo yalihusu maendeleo ya Taasisi ya Uongozi iliyoanzishwa
na Serikali za Tanzania na Finland mwaka 2010 kwa lengo la kuwajengea Viongozi
wa Tanzania na Afrika, uwezo wa kumudu majukumu yao vema na kwa ufanisi zaidi.
Katibu
Mkuu Kiongozi aliishukuru Serikali ya Finland kwa kuendelea kuwa mbia muhimu wa
maendeleo wa Tanzania, sio tu kupitia Taasisi ya Uongozi bali pia kupitia
miradi mbalimbali inayoifadhili nchini. Alisema uwekezaji wa Serikali zetu
mbili umeiwezesha Taasisi ya Uongozi kupata mafanikio na heshima kubwa barani
Afrika na duniani. Aliongeza kuwa, ndio maana nchi hizo zimedhamiria kuwekeza
zaidi na kufungua milango kwa wabia wengine, ili kuimarisha Taasisi hiyo na
kuiwezesha kuhudumia washiriki kutoka katika nchi nyingi za Afrika.
Kuhusu
uwekezaji wa Serikali ya Tanzania katika Taasisi ya Uongozi, Katibu Mkuu
Kiongozi alizungumzia uamuzi wa Serikali wa kutoa kiwanja kwa ajili ya kujenga
maskani ya kudumu ya Taasisi hiyo katika mji wa Bagamoyo. Vilevile, alibainisha
kuwa Serikali ya Tanzania inachangia zaidi ya asilimia 40 za gharama za
uendeshaji wa Taasisi hiyo. Aliongeza pia, katika jitihada za kuhakikisha kuwa Taasisi
ni mradi endelevu, Serikali imepeleka zaidi ya Watumishi 1,600 kupata mafunzo
katika Taasisi hiyo.
Kwa
upande wa Serikali ya Finland, Balozi Alanko alisema kuwa pamoja na mikakati ya
kubana matumizi, Serikali mpya ya nchi hiyo, iliyoingia madarakani mwezi Juni,
2015, imetoa kipaumbele kwa Tanzania kuendelea kupata misaada ya maendeleo na
fursa kwa makampuni ya Finland kuwekeza nchini. Aidha, ameahidi kuwa Bodi ya
Taasisi ya Uongozi itaendelea kushirikiana na Menejimenti ya Taasisi
kuhakikisha kuwa inatekeleza matakwa ya nchi washirika (Tanzania na Finland).
Kwa sasa Bodi hiyo na wadau wake, ipo katika mchakato wa kuandaa Mpango Mkakati wa miaka mitano 2016/17 – 2021/22 ambao utalenga kupanua wigo wa huduma za Taasisi hiyo, ili kuzifikia nchi nyingi zaidi za Afrika na kuweka msisitizo katika utekelezaji wa Malengo ya Maendeleo Endelevu (SDGs), hususan katika eneo la Utawala Bora.