Tanzania emblem
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Ofisi ya Katibu Mkuu Kiongozi

Habari

Katibu Mkuu Kiongozi atembelea Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Dodoma na kukagua maendeleo ya mradi wa ujenzi wa ofisi mpya za Mkuu wa Mkoa wa Dodoma. 7 Septemba, 2016


Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi Mhandisi John W. H. Kijazi, leo tarehe 7 Septemba, 2016 ametembelea Ofisi za Mkuu wa Mkoa wa Dodoma na baadaye alipata fursa ya kutembelea mradi wa ujenzi wa Ofisi mpya za Mkuu wa Mkoa iliyopo eneo la Kilimani mjini Dodoma.

Akiwa katika Ofisi za Mkuu wa Mkoa, Katibu Mkuu Kiongozi alipokea taarifa ya Mkuu wa Mkoa, Mheshimiwa Jordan Rugimbana kuhusu maandalizi ya Serikali kuhamia Dodoma, ambapo Mkuu wa Mkoa alitaarifu kuwa maandalizi yanaendelea vizuri na kwamba Uongozi wa Mkoa na Wananchi wa Dodoma wamejipanga vilivyo kupokea wageni mbalimbali kutoka Dar es Salaam na maeneo mengine ya Tanzania watakaohamia Dodoma.

Kikao hicho kifupi kiliudhuriwa pia na Katibu Tawala wa Mkoa pamoja na Wajumbe wengine wa Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Mkoa wa Dodoma. Akiongea katika Kikao hicho, Katibu Mkuu Kiongozi aliwapongeza kwa maandalizi hayo na kuahidi kuendelea kuwapatia ushirikiano. Aidha, alisisitiza umuhimu wa uratibu mahiri wa wadau wote wanaoshiriki katika mchakato wa maandalizi ya Serikali kuhamia Dodoma ili kupata matokeo makubwa zaidi katika maeneo yote ya mpango huo.

Baada ya kumalizika kwa Kikao hicho, Katibu Mkuu Kiongozi alitembelea mradi wa ujenzi wa Ofisi mpya za Mkuu wa Mkoa inayojengwa katika eneo la Kilimani mjini Dodoma. Akiwa katika mradi huo Katibu Mkuu Kiongozi alieleza kufurahishwa kwake na ubunifu wa jengo hilo pamoja na hatua iliyofikiwa katika ujenzi huo. Aidha, alimwahidi Mkuu wa Mkoa kuwa Ofisi yake itatoa ushirikiano utakaohitajika ili kuhakikisha ujenzi huo unakamilika mapema.

Kufuatia ziara hiyo Katibu Mkuu Kiongozi, alifanya ziara nyingine kwenye Kituo cha Taifa cha Kumbukumbu na Nyaraka kilichopo eneo la Kisasa mjini Dodoma ambapo alipata wasaa wa kukutana na kufanya mazungumzo na Viongozi na Wafanyakazi wa Kituo hicho. Mazungumzo hayo pia yalimshirikisha Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais Menejiment ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Dkt. Laurean Ndumbaro na Kaimu Mkurugenzi wa Kituo cha Kumbukumbu Tuli, Bwana Firimin M. Msiangi.

Katibu Mkuu Kiongozi aliupongeza Uongozi na Wafanyakazi wa Kituo hicho kwa kazi nzuri wanayoendelea kuifanya katika utekelezaji wa majukumu yao. Aidha, alisisitiza umuhimu wa kuweka kumbukumbu muhimu kwa ajili ya matumizi ya sasa na baadaye ya Serikali. Vilevile, aliwakumbusha watumishi wote kituoni hapo umuhimu wa kudumisha uadilifu na maadili, ikiwa ni pamoja na kutunza siri za nyaraka zinazochujwa na kutunzwa kituano hapo . Kadhalika, alisisitiza umuhimu wa Wizara, Idara na Taasisi za Serikali kukitumia Kituo hicho kama ilivyokusudiwa. Mwisho aliahidi kuwa Serikali itajitahidi kuzitafutia ufumbuzi changamoto mbalimbali zinazokikabili Kituo hicho na watumishi wake.