Tanzania emblem
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Ofisi ya Katibu Mkuu Kiongozi

Habari

Katibu Mkuu Kiongozi atembelea na kukagua eneo utakapojengwa Mji wa Kisasa wa Serikali, Ihumwa Mjini Dodoma. 23/11/2017


KATIBU MKUU KIONGOZI ATEMBELEA NA KUKAGUA ENEO UTAKAPOJENGWA MJI WA KISASA WA SERIKALI, IHUMWA MJINI DODOMA. 23/11/2017

Na Frank Mvungi- Maelezo, Dodoma

Katibu Mkuu Kiongozi Balozi Mhandisi John Kijazi na Makatibu Wakuu leo wametembelea na Kukagua eneo utakapojengwa Mji wa Kisasa wa Serikali katika eneo la Ihumwa Mjini Dodoma, ili kujionea hatua zilizofikiwa katika utekelezaji wa mradi huo.

Akizungumza katika eneo la mradi unaotarajiwa kutekelezwa katika eneo lenye ukubwa ekari 1500 Balozi Kijazi amesema kuwa Mji huo utakuwa wa kipekee na hiyo ni sehemu ya mikakati ya Serikali kuhakikisha kuwa Makao Makuu ya nchi yanakuwa katika mpangilio wa kisasa ili kuleta tofauti kati ya mji huo na miji mingine.

“Niwatoe wananchi shaka kuhusu Serikali kuhamia Dodoma kwa kuwa dhamira ya Serikali ya Awamu ya Tano inayoongozwa na Mhe. Rais Dkt. John Pombe Magufuli imeshaanza kutekelezwa kwa vitendo na sehemu kubwa ya Watumishi wa Serikali wameshahamia hapa Dodoma Wakiwemo Mawaziri na Makatibu Wakuu” . Alisisitiza Balozi Kijazi

Akifafanua amesema kuwa mji huo utakuwa na maeneo kwa ajili ya majengo ya Wizara, Taasisi, Balozi, na huduma mbalimbali za kijamii ikiwemo Viwanja vya michezo, Hospitali, maeneo ya kupumzikia, Maeneo ya Biashara .

Aliongeza kuwa upatikanaji wa huduma katika Mji wa Serikali utakuwa wa uhakika na utakuwa umerahisishwa kutokana na kuwepo kwa Taasisi za Serikali na Wizara zote katika eneo moja.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Nyumba la Taifa Bw. Nehemia Mchechu amesema kuwa ni muhimu kuvutia wawekezaji kuja kuwekeza mkoani Dodoma kutokana na mipango ya Serikali kujenga mji huo wa Kisasa wa Serikali.

Aliongeza kuwa mawazo ya awali ya namna ya kujenga mji huo wa kisasa wa Serikali yapo na kinachosubiriwa ni hatua mbalimbali za kiutendaji zitakazowezesha kutekelezwa kwa mradi huo.

Uamuzi wa Serikali kuhamia Dodoma umepata msukumo katika kipindi cha Serikali ya Awamu ya Tano inayoongozwa na Rais Dkt. John Pombe Magufuli na tayari utekelezaji wake unaendelea ambapo Mawaziri wote wameshahamia Dodoma, Makatibu Wakuu na Watumishi Wengine wa Serikali pia wameshahamia.