Tanzania emblem
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Ofisi ya Katibu Mkuu Kiongozi

Habari

Katibu Mkuu Kiongozi ashiriki katika kipindi cha Tunatekeleza TBC - 06 Februari, 2017


Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi., Mhandisi John H. W. Kijazi leo tarehe 06 Februari, 2017 ameshiriki katika kipindi cha Televisheni cha TUNATEKELEZA kilichoandaliwa na Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo kupitia Idara ya Habari Maelezo na kurushwa mubashara kwa takriban dakika 45 na kituo cha Televisheni cha Shirika la Utangazaji la Taifa (TBC).

Katika kipindi hicho, kilichoongozwa na Bw. Rashid Salim wa TBC, Katibu Mkuu Kiongozi alielezea kwa ufupi, majukumu anayoyatekeleza akiwa Mkuu wa Utumishi wa Umma, Mshauri wa Rais wa masuala yote yanayohusu nidhamu na utendaji Serikalini na Katibu wa Baraza la Mawaziri.

Katibu Mkuu Kiongozi, alizungumzia pia hatua mbalimbali zilizochukuliwa na zinazoendelea kuchukuliwa na Serikali ya Awamu ya Tano katika kuimarisha utendaji kazi serikalini, kusimamia nidhamu, uadilifu na uwajibikaji miongoni mwa watumishi wa umma. Aidha, alifafanua kuhusu zoezi la uhakiki wa vyeti vya Kidato cha Nne (4), Kidato cha Sita (6) na ualimu vya watumishi wa umma linaloendelea hadi kufikia mwishoni mwa mwezi Februari, 2017.

Suala lingine alilolizungumzia ni kuhusu hatua za Serikali ya Awamu ya Tano la kudhibiti matumizi ya fedha za umma, ambapo alitoa mifano mbalimbali ikiwemo kuhusu fedha zilizookolewa baada ya kuhairishwa kwa sherehe za maadhimisho ya sikukuu za kitaifa na nyinginezo. Katibu Mkuu Kiongozi alibainisha kuwa badala ya matumizi hayo, fedha hizo zilielekezwa katika kufanikisha miradi ya kipaumbele na kutatua kero za wananchi.

Sambamba na hayo Katibu Mkuu Kiongozi alizungumzia pia hatua zinazochukuliwa na Serikali ya Awamu ya Tano katika kuimarisha ukusanyaji wa mapato wenye lengo la kuiwezesha Serikali kujitegemea na kufanikisha miradi yake, ikiwemo ya kimkakati kwa fedha za ndani. Vilevile, alizungumzia hatua zilizolenga kupunguza urasimu na kuongeza ufanisi katika utoaji wa huduma kwa wananchi na sekta binafsi ambayo ni mhimili muhimu kwa uchumi wa taifa.

Katibu Mkuu Kiongozi alizungumzia pia jitihada za Serikali ya Awamu ya Tano katika kukuza uchumi wa nchi, ikiwa ni pamoja na kuimarisha sekta za kimkakati kama vile viwanda, ujenzi, uchukuzi, mawasiliano, kilimo, elimu, afya, nishati, maji n.k. Kuhusu sekta ya uchukuzi, alizungumzia utatuzi wa kero katika utolewaji huduma katika bandari ya Dar es Salaam na uimarishaji wa sekta ya usafiri wa anga nchini, ambapo mabadiliko makubwa yamefanyika katika uongozi wa Shirika la Ndege la Taifa (ATCL) na Serikali inatekeleza mpango kapambe wa kununua ndege mpya kwa ajili ya Shirika hilo ili iweze kuchangia zaidi kwenye uchumi wa taifa na kutoa huduma bora kwa wananchi. Aidha, alizungumzia utatuzi wa kero zilizokuwepo kuhusu vituo vya ukaguzi wa magari ya mizigo yanayokwenda nje ya nchi kutokea bandarini, ambapo vituo vya ukaguzi vimepunguzwa kufikia vitatu (3) kwa Ukanda wa Kati na vinne (4) kwa Ukanda wa Dar es Salaam. Kuhusu viwanda alitoa mifano michache ya viwanda vikubwa vilivyojengwa na vinavyokusudiwa kujengwa, vitakavyowezesha kutimia kwa dhima ya uchumi wa viwanda.

Katibu Mkuu Kiongozi aliongelea masuala mengine muhimu ikiwa ni pamoja na mchakato wa Serikali kuhamia Dodoma, ambapo aliweka bayana kuwa baadhi Wizara zimeshaanza kuhamia katika Makao Makuu ya Serikali, na nyingine zitatekeleza suala hilo kwa awamu bila kuathiri utendaji kazi Serikalini. Hali kadhalika, Katibu Mkuu Kiongozi alizungumzia na kufafanua kuhusu utekelezaji wa Mpango wa Pili wa Maendeleo kwa kipindi cha Miaka Mitano kuanzia 2016/17 hadi 2020/21 na Dira ya Taifa ya Maendeleo hadi kufikia mwaka 2025.

Mwishoni mwa kipindi hicho, Katibu Mkuu Kiongozi alitoa wito kwa Wananchi kwa ujumla kuunga mkono juhudi zinazofanywa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. John Pombe Joseph Magufuli na Serikali yake katika kutekeleza ahadi, mikakati na mipango mbalimbali kwa manufaa ya wananchi wote.

Kabla ya kushiriki kwenye kipindi hicho, Katibu Mkuu Kiongozi alikutana na kufanya mazungumzo na Mtendaji Mkuu wa TBC Dkt. Ayub Rioba kuhusu mustakabali na maono ya Shirika hilo.