Tanzania emblem
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Ofisi ya Katibu Mkuu Kiongozi

Habari

Katibu Mkuu Kiongozi amuwakilisha Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwenye ufunguzi wa Maadhimisho ya 15 ya siku ya Wahandisi Tanzania, Dodoma, 7 Septemba, 2017


Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi Mha. John W.H. Kijazi, leo tarehe 7 Septemba, 2017 amemwakilisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. John Pombe Joseph Magufuli katika ufunguzi wa Maadhimisho ya 15 ya Siku ya Wahandisi Tanzania yanayofanyika katika Ukumbi wa Mikutano wa Dkt. Jakaya Kikwete, mjini Dodoma kwa muda wa siku mbili, tarehe 7 -8 Septemba, 2017.

Maadhimisho hayo yaliyoandaliwa na Bodi ya Usajili wa Wahandisi Tanzania (Engineers Registration Board) na Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano yana mada kuu isemayo “Jukumu la Sayansi, Teknolojia, Uhandisi na Hisabati katika kukuza Viwanda kwa Maendeleo ya Kijamii na Kiuchumi.”

Katika siku mbili za Mkutano huo, Wahandisi wapatao takriban 2,000 kutoka sehemu mbalimbali nchini wanajadili masuala mbalimbali kuhusu taaluma ya Uhandisi zikiwemo changamato na fursa za Wahandisi katika utekelezaji wa Mpango wa Pili wa Maendeleo wa Taifa wa Miaka Mitano (2016/17 – 2020/21). Aidha, watashiriki katika maonesho ya kiufundi na kibiashara yanayoonesha bidhaa zinazotokana na ubunifu wa kihandisi.

Katika hotuba yake ya ufunguzi, Katibu Mkuu Kiongozi aliishukuru Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Bodi ya Usajili wa Wahandisi Mawasiliano kwa mwaliko wa kuhudhuria maadhimisho hayo ambayo yamefanyika kwa mara ya kwanza Mjini Dodoma, Makao Makuu ya Nchi na Serikali. Aidha, aliipongeza Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano kwa kuandaa maadhimisho hayo na kuchagua mada kuu inayoakisi azma ya Serikali ya Awamu ya Tano ya kujenga uchumi wa viwanda na kuzipatia ufumbuzi changamoto za msingi za Watanzania, hususan walio maskini.

Katibu Mkuu Kiongozi alisisitiza kuwa Tanzania, kama zilivyo nchi nyingine duniani inategemea Wanasayansi kubuni mbinu za kukabiliana na changamoto mbalimbali za kimaendeleo. Aidha, alikiri kuwa Serikali inafahamu kuhusu idadi isiyokidhi ya Wahandisi na kutaja hatua mbalimbali zinazochukuliwa ili kuongeza idadi hiyo ikiwa ni pamoja na kuboresha elimu ya sekondari na kuhamasisha vijana wasome masomo ya sayansi; kuongeza nafasi za masomo ya Uhandisi katika Vyuo vikuu; na kuongeza idadi ya Wasichana wanaosoma Uhandisi katika vyuo vikuu na vyuo vya mafunzo ya ufundi.

Kuhusu ushiriki wa Wahandisi wa ndani katika utekelezaji wa miradi ya ndani, Katibu Mkuu Kiongozi alisisita umuhimu wa utayari na uwezo wao ambavyo ndio vitakaowawezesha kuwania fursa zilizopo na zitakazokuwepo na kuhimili ushindani katika tasnia hiyo. Katika suala la kuwajengea utayari na uwezo Wahandisi wa ndani, Katibu Mkuu Kiongozi aliishukuru Bodi ya Usajili wa Wahandisi na wadau wengine, ukiwemo Ubalozi wa Norway unafadhili mafunzo kwa vitendo kwa Wahandisi Wahitimu wanawake na Benki ya Dunia inayofadhili mafunzo hayo kupitia mradi wa “Dar es Salaam Urban Transport Improvement Project.”

Katika hotuba hiyo pia, Katibu Mkuu Kiongozi alisisitiza umuhimu wa ushirikiano baina ya Sekta ya Umma na Binafsi na miongoni mwa Wizara, Idara na Taasisi za Serikali. “Hivyo, rai yangu kubwa kwenu ni kwa wadau wote kutoka Sekta Binafsi na ya Umma kudumisha ushirikiano katika kufanikisha ujenzi wa Tanzania ya Viwanda” alisema.

Akiongea kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Mkuu wa Wilaya ya Chemba, Mheshimiwa Simon Odunga aliwakaribisha Wahandisi Mjini Dodoma, Makao Makuu ya Nchi na Serikali. Aidha, aliwafahamisha kuwa Dodoma inazo fursa mbalimbali kwa Wahandisi kufuatia uamuzi wa Serikali wa kuhamia Dodoma.

Naye Mwenyekiti wa Bodi ya Usajili wa Wahandisi, Mha. Prof. Ninatubu Lema alimshukuru sana Katibu Mkuu Kiongozi kwa kukubali mwaliko wa Bodi na kuelezea furaha waliyokuwa nayo Wahandisi kwa kuwa naye katika Maadhimisho hayo, kuzingatia taaluma yake ya Uhandisi. Aidha, alieleza azma ya Wahandisi kushiriki kikamilifu katika ujenzi wa uchumi wa Viwanda nchini Tanzania na kutatua changamoto zinazowakabili Wahandisi. Vilevile aliiomba Serikali kupitia kwa Katibu Mkuu Kiongozi kuruhusu miradi mikubwa ya ujenzi wa miundombinu ya reli, barabara, viwanja vya ndege, bandari na mabomba ya usafirishaji wa mafuta na gesi asilia itumike kama madarasa kwa Wahandisi vijana; iweke utaratibu mzuri wa kuwajengea uwezo Wahandisi wa ndani kwa kutoruhusu kampuni za kandarasi kutoka nchi za nje kutofanya kazi nchini bila ya ubia na makampuni ya ndani; na ipige marufuku uingizwaji wa vifaa vya ujenzi ambavyo vinazalishwa na viwanda vya ndani.

Katibu Mkuu Kiongozi alipokea maombi hayo na kuhaidi kuwa Serikali itayafanyia kazi pindi yatakapowasilishwa rasmi na Bodi ya Usajili wa Wahandisi.