Tanzania emblem
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Ofisi ya Katibu Mkuu Kiongozi

Habari

Katibu Mkuu Kiongozi ameongoza Mkutano wa Kamati Maalum ya Makatibu Wakuu na Vikao vya Kazi vya Makatibu Wakuu wa Wizara zote hapa Dodoma 01 Machi, 2017.


Katibu Mkuu Kiongozi ameongoza Mkutano wa Kamati Maalum ya Makatibu Wakuu na Vikao vya Kazi vya Makatibu Wakuu wa Wizara zote hapa Dodoma 01 Machi, 2017.

Leo tarehe 1 Machi, 2017 Katibu Mkuu Kiongozi ambaye pia ni Katibu wa Baraza la Mawaziri, Balozi Mha. John W. H. Kijazi ameongoza Mkutano wa Kamati Maalum ya Makatibu Wakuu na Vikao vya Kazi vya Makatibu Wakuu wa Wizara zote hapa Dodoma.

Hii ni mara ya Kwanza kwa Mkutano na Vikao hivyo kufanyika mjini Dodoma tangu Serikali ya Awamu ya Tano ifanye uamuzi wa kuhamia Dodoma.

Vikao hivyo vitakavyodumu kwa siku tatu (3) vitapokea na kujadili agenda mbalimbali zitakazowasilishwa na Wizara, zinazohusu masuala ya takwimu; ujenzi wa miundombinu; miradi mikubwa ya kimkakati ikiwemo ya sekta ya mafuta na gesi; mazingira ya uwekezaji na biashara na namna ya kukabiliana na changamoto zake.

Kamati Maalum ya Makatibu Wakuu ndicho chombo Kikuu cha Kitaalam chenye jukumu la kupokea, kuchambua na kujadili nyaraka mbalimbali zinazowasilishwa na Wizara kabla hazifikishwa kwenye Baraza la Mawaziri kwa mijadala na maamuzi.

Tangu Serikali ya Awamu ya Tano iingie madarakani, Baraza la Mawaziri limeshakutana mara 13 na kufanya maamuzi makubwa na muhimu kwa mustakabali wa Tanzania na Watanzania, ukiwemo uamuzi muhimu kuhusu ujenzi wa Bomba la Mafuta kutoka Hoima nchini Uganda hadi Bandari ya Tanga.

Katika mazungumzo yao yaliyofanyika tarehe 25 Februari, 2017, Marais wa Uganda na Tanzania walielezea dhamira yao ya kuhakikisha mradi huo unatekelezwa bila ya kuchelewa.

Mkutano wa Kamati Maalum wa Makatibu Wakuu wa Wizara zote ni kielelezo dhahiri cha utekelezaji kwa vitendo azma ya Serikali kuhamia Dodoma. Hadi kufikia tarehe 1 Machi, 2017 takriban Wizara zote za Serikali zilikuwa zimeshahamia Dodoma. Zoezi hili muhimu lilizinduliwa rasmi na Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Kassim M. Majaliwa (MB) mnamo tarehe 30 Septemba, 2016.

Ofisi ya Katibu Mkuu Kiongozi inawashukuru Watanzania wote kwa kuendelea kuunga mkono jitihada mbalimbali za Serikali ya Awamu ya Tano zenye lengo la kujenga Tanzania mpya yenye maendeleo zaidi kwa watu wote na uchumi imara unaotegemea Viwanda.

Aidha, inatoa rai kwa wananchi na watu wote kuzitumia kikamilifu fursa mbalimbali zilizopo katika Mji Mkuu wa Tanzania na Makao Makuu ya Serikali –Dodoma, ambazo zimehuishwa kufuatia uamuzi huu muhimu wa Serikali. Fursa hizo ni pamoja na biashara na uwekezaji; na huduma mbalimbali za kiuchumi na kijamii. PAMOJA TUJENGE TANZANIA MPYA.

Imetolewa na Ofisi ya Katibu Mkuu Kiongozi

01/03/2017

DODOMA