Tanzania emblem
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Ofisi ya Katibu Mkuu Kiongozi

Habari

Katibu Mkuu Kiongozi akutana na Wakuu wa Wilaya na Wakurugenzi wa Mamlaka za Serikali za Mitaa Mjini Dodoma, 14 Septemba, 2017


Leo tarehe 14 Septemba, 2017, Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi Mha. John W.H. Kijazi amefanya Mkutano na Wakuu wa Wilaya na Wakurugenzi wa Mamlaka za Serikali za Mitaa wanaohudhuria mafunzo ya siku tano (5) yanayoendeshwa na Ofisi ya Rais – TAMISEMI kwa ushirikiano na Taasisi ya Uongozi, katika Ukumbi wa Hazina Square, mjini Dodoma.

Mafunzo hayo ya Uongozi yaliyoanza tangu Jumatatu tarehe 11 Septemba, 2017 na ambayo yanatarajiwa kuhimitimishwa siku ya Ijumaa, tarehe 15 Septemba, 2017, yanahusisha Wakuu wa Wilaya na Wakurugenzi wa Serikali za Mitaa wapatao 84 kutoka katika Mikoa ya Dar es Salaam, Mbeya, Njombe, Shinyanga, Iringa, Ruvuma, Songwe na Rukwa. Mafunzo kama hayo yalitolewa pia katika awamu zilizotangulia kwa Wakuu wa Wilaya na Wakurugenzi wa Serikali za Mitaa kutoka mikoa ya Dodoma, Singida, Morogoro, Tabora, Kigoma, Katavi, Mwanza, Mara, Geita, Simiyu, Manyara na Kagera.

Akimkaribisha Katibu Mkuu Kiongozi kuzungumza na washiriki wa mafunzo hayo, Naibu Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais – TAMISEMI, anayesimamia Afya, Dkt. Zainab Chaula alieleza umuhimu wa mafunzo hayo ya aina yake, yanayotolewa kwa Wakuu wa Wilaya na Wakurugenzi wa Mamlaka za Serikali za Mitaa kutoka Mikoa yote ya Tanzania Bara. Alibainisha kuwa lengo kuu la mafunzo hayo ni kuwaongezea uelewa wa masuala mbalimbali ya kiutawala, kiutumishi na mengineyo ambayo yanahusu utekelezaji wa majukumu yao ya kazi za kila siku.

Akiongea na washiriki wa mafunzo hayo, Katibu Mkuu Kiongozi aliwahimiza washiriki wa mafunzo hayo wasome, kuzielewa na kuzizingatia Sheria, Kanuni na Miongozo mbalimbali inayohusika na masuala ya Kiutawala na Kiutumishi ili kupata uelewa mzuri utakaowawezesha kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi zaidi. Sheria na Kanuni hizo ni pamoja na zile za Mamlaka za Serikali za Mitaa; Sheria ya Utumishi wa Umma na Kanuni zake; Sheria ya Fedha za Umma na Kanuni zake; Sheria ya Ununuzi wa Umma na Kanuni zake; na nyinginezo.

Katibu Mkuu Kiongozi pia aliwasihi wawe karibu na wananchi, wawasikilize na kutatua changamoto mbalimbali zinazowakabili, kwa kutambua kuwa lengo kuu la Serikali katika ngazi yoyote ni ustawi wa wananchi na kwamba Serikali inawajibika kwa wananchi wake.

Akiongelea umuhimu wa udhibiti wa mapato ya Serikali za Mitaa na matumizi ya fedha za umma, Katibu Mkuu Kiongozi aliwaagiza washiriki wa mafunzo hayo na Uongozi wa TAMISEMI kufanyia kazi mapungufu yaliyobainishwa katika Ripoti ya Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Fedha za Serikali, ikiwemo ya mwaka wa fedha 2015/ 2016.

Katibu Mkuu Kiongozi alizungumzia pia masuala yanayogusa sekta mbalimbali zikiwemo za Maji, Nishati na Madini, Ardhi, Ujenzi na Viwanda na Biashara, ambapo alitoa maelekezo mahsusi kwa washiriki wa mafunzo hayo na Mamlaka za Serikali za Mitaa kwa ujumla.

Kwa upande wao, washiriki wa mafunzo walimshukuru Katibu Mkuu Kiongozi wa kutenga muda wake kukutana nao na kwa maelekezo yake ya kina ambayo wameahidi kuyazingatia.